Tuesday, September 8, 2015

ZIJUE FAIDA ZA TANGO

MATANGO

Mwili wa binadamu ili uweze kuwa katika afya nzuri, unahitaji kuwa na virutubisho vya kutosha. Virutubisho hivi tunavipata katika vyakula, matunda na hata kupitia katika vinywaji mbalimbali tunaweza kupata vitu muhimu kwa ajili ya afya zetu.
Mpenzi msomaji, leo napenda kukufahamisha au kukukumbusha kuhusu faida zinazotokana na ulaji wa tunda hili maarufu sana, TANGO.
Miongoni mwa faida tunazozipata kwa kula matango ni hizi zifuatazo:
Kwanza kabisa, ulaji wa matango husaidia kuboresha kiwango cha maji ambayo huitajika mwilini, hii ni kutokana na matango kuwa na kiwango kikubwa cha maji. Maji haya husaidia kuondoa taka mwili pamoja na sumu mbalimbali ambazo miili yetu huzipata kupitia vyakula, madawa na hata vinywaji.
Pili, husaidia kupunguza uzito wa mwili. Kutokana na matango kuwa na asili ya nyuzi nyuzi au, fibres, humfanya mlaji ajisikie kushiba bila ya kuongeza vitu mwilini ambavyo husababisha mtu aongezeke uzito.
Tatu, hupunguza (hangovers),uchovu, mawengewenge pamoja na hali ya kujisikia vibaya kutokana na unywaji wa kilevi. Hii ni kutokana na kuwa na vitamini B na maji mengi ambapo, baada ya mtu kunywa kilevi na kisha akaja kula matango kabla ya kulala, itamfanya asubuhi asiamke huku akiwa na hangovers.
Nne,husaidia katika mmeng’enyo wa chakula, matatizo ya tumbo kama vile kuvimbiwa, tumbo kujaa gesi, vidonda vya tumbo na mengineyo hupungua kutokana na ulaji wa matango, husaidia kuondoa sumu tumboni na kurahisisha ufyonzwaji wa protein mwilini kutokana na uwepo wa kiwezeshaji cha kibaiolojia kinachoitwa, erepsin enzyme.
Tano, husaidia kuondoa msongo wa mawazo. Matango yana kiwango kikubwa cha vitamini B ambayo husaidia kuboresha utendaji kazi wa mishipa mbalimbali ya fahamu mwilini na hivyo kuondoa hatari ya mtu kuathirika na msongo wa mawazo unaosababishwa na maisha ya kila siku.
Sita, husaidia kuondoa hatari ya mtu kupata kansa. Yana kiwango kikubwa cha virutubisho vyenye asili ya mimea viitwavyo, lignans, ambavyo pamoja na vitamini c, husaidia kuondoa sumu mbalimbali na kuiboresha kinga ya mwili na hivyo kuepusha hatari ya mtu kupata kansa.
Saba, husaidia kuondoa harufu mbaya kinywani. Kwa kukiweka kipande cha tango mdomoni kwa dakika kadhaa, huuwa bakteria mbalimbali wasababishao magonjwa mbalimbali ya kinywa na harufu mbaya mdomoni.
Mpenzi msomaji, tunakushukuru kwa kuendelea kuwa nasi katika blog hii, tutazidi kukuletea dondoo mbalimbali za afya na usisite kuwasiliana nasi endapo utakuwa na maoni au jambo lolote la kutushirikisha juu ya afya zetu.

shudate blog

0 comments:

Post a Comment